Biblica® Open Kiswahili Contemporary Version (Neno) 2015

Mika 6:1-16

Shauri La Bwana Dhidi Ya Israeli

1Sikiliza asemalo Bwana:

“Simama, tetea shauri lako mbele ya milima;

vilima na visikie lile unalotaka kusema.

2Sikilizeni, ee milima, mashtaka ya Bwana,

sikilizeni, enyi misingi ya milele ya dunia.

Kwa kuwa Bwana ana shauri dhidi ya watu wake;

anatoa mashtaka dhidi ya Israeli.

3“Watu wangu, nimewatendea nini?

Nimewalemea kwa jinsi gani? Mnijibu.

4Nimewatoa kutoka Misri na kuwakomboa

kutoka nchi ya utumwa.

Nilimtuma Mose awaongoze,

pia Aroni na Miriamu.

5Watu wangu, kumbukeni jinsi Balaki mfalme wa Moabu

alivyofanya shauri

na kile Balaamu mwana wa Beori alichojibu.

Kumbukeni safari yenu kutoka Shitimu mpaka Gilgali,

ili mfahamu matendo ya haki ya Bwana.”

6Nimjie Bwana na kitu gani na kusujudu

mbele za Mungu aliyetukuka?

Je, nije mbele zake na sadaka za kuteketezwa,

nije na ndama za mwaka mmoja?

7Je, Bwana atafurahishwa na kondoo dume elfu,

au mito elfu kumi ya mafuta?

Je, nimtoe mzaliwa wangu wa kwanza kwa ajili ya kosa langu,

mtoto wangu mwenyewe

kwa ajili ya dhambi ya nafsi yangu?

8Amekuonyesha yaliyo mema, ee mwanadamu.

Bwana anataka nini kwako?

Ila kutenda kwa haki na kupenda rehema,

na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako.

Hatia Na Adhabu Ya Israeli

9Sikiliza! Bwana anauita mji:

kulicha jina lako ni hekima:

“Tii hiyo fimbo na yeye aliyeiamuru.

10Je, bado nisahau, ee nyumba ya uovu,

hazina yako uliyopata kwa udanganyifu

na vipimo vilivyopunguka,

ambavyo vimelaaniwa?

11Je, naweza kuhukumu kuwa

mtu mwenye mizani ya udanganyifu hana hatia,

aliye na mfuko wa mawe ya kupimia ya uongo?

12Matajiri wake ni wajeuri;

watu wake ni waongo

na ndimi zao zinazungumza

kwa udanganyifu.

13Kwa hiyo, nimeanza kukuharibu,

kuwaangamiza kwa sababu ya dhambi zenu.

14Mtakula lakini hamtashiba;

matumbo yenu bado yatakuwa matupu.

Mtaweka akiba lakini hamtaokoa chochote,

kwa sababu mtakachoweka akiba

nitatoa kwa upanga.

15Mtapanda lakini hamtavuna;

mtakamua zeituni lakini

hamtatumia mafuta yake.

Mtakamua zabibu

lakini hamtakunywa hiyo divai.

16Mmezishika sheria za Omri

na matendo yote ya nyumba ya Ahabu,

tena umefuata desturi zao.

Kwa hiyo nitakutoa kwa maangamizi

na watu wako kuwa dhihaka;

mtachukua dharau za mataifa.”