Biblica® Open Kiswahili Contemporary Version (Neno) 2015

Zaburi 144:1-15

Zaburi 144

Mfalme Amshukuru Mungu Kwa Ushindi

Zaburi ya Daudi.

1Sifa ni kwa Bwana Mwamba wangu,

aifundishaye mikono yangu vita,

na vidole vyangu kupigana.

2Yeye ni Mungu wangu wa upendo na boma langu,

ngome yangu na mwokozi wangu,

ngao yangu ninayemkimbilia,

ambaye huwatiisha mataifa chini yangu.

3Ee Bwana, mwanadamu ni nini hata umjali,

Binadamu ni nini hata umfikirie?

4Mwanadamu ni kama pumzi,

siku zake ni kama kivuli kinachopita.

5Ee Bwana, pasua mbingu zako, ushuke,

gusa milima ili itoe moshi.

6Peleka umeme uwatawanye adui,

lenga mishale yako uwashinde.

7Nyoosha mkono wako kutoka juu,

nikomboe na kuniokoa

kutoka maji makuu,

kutoka mikononi mwa wageni

8ambao vinywa vyao vimejaa uongo,

na mikono yao ya kuume ni midanganyifu.

9Ee Mungu, nitakuimbia wimbo mpya,

kwa zeze yenye nyuzi kumi nitakuimbia,

10kwa Yule awapaye wafalme ushindi,

ambaye humwokoa Daudi, mtumishi wake kutokana na upanga hatari.

11Nikomboe na uniokoe

kutoka mikononi mwa wageni

ambao vinywa vyao vimejaa uongo,

na mikono yao ya kuume ni midanganyifu.

12Kisha wana wetu wakati wa ujana wao

watakuwa kama mimea iliyotunzwa vizuri,

binti zetu watakuwa kama nguzo zilizoviringwa

kurembesha jumba la kifalme.

13Ghala zetu zitajazwa

aina zote za mahitaji.

Kondoo zetu watazaa kwa maelfu,

kwa makumi ya maelfu katika mashamba yetu;

14maksai wetu watakokota

mizigo mizito.

Hakutakuwa na kubomoka kuta,

hakuna kuchukuliwa mateka,

wala kilio cha taabu

katika barabara zetu.

15Heri watu ambao hili ni kweli;

heri wale ambao Bwana ni Mungu wao.