Biblica® Open Kiswahili Contemporary Version (Neno) 2015

Zaburi 146:1-10

Zaburi 146

Kumsifu Mungu Mwokozi

1Msifuni Bwana!146:1 Msifuni Bwana kwa Kiebrania ni Hallelu Yah.

Ee nafsi yangu, umsifu Bwana,

2Nitamsifu Bwana maisha yangu yote;

nitamwimbia Mungu wangu sifa

wakati wote niishipo.

3Usiweke tumaini lako kwa wakuu,

kwa wanadamu ambao hufa,

ambao hawawezi kuokoa.

4Roho yao itokapo hurudi mavumbini,

siku hiyo hiyo mipango yao yote hukoma.

5Heri yeye ambaye Mungu wa Yakobo ni msaada wake,

ambaye tumaini lake ni katika Bwana, Mungu wake,

6Muumba wa mbingu na nchi,

na bahari na vyote vilivyomo ndani yake:

Bwana anayedumu kuwa mwaminifu

milele na milele.

7Naye huwapatia haki walioonewa

na kuwapa wenye njaa chakula.

Bwana huwaweka wafungwa huru,

8Bwana huwafumbua vipofu macho,

Bwana huwainua waliolemewa na mizigo yao,

Bwana huwapenda wenye haki.

9Bwana huwalinda wageni

na kuwategemeza yatima na wajane,

lakini hupinga njia za waovu.

10Bwana atamiliki milele,

Mungu wako, ee Sayuni,

kwa vizazi vyote.

Msifuni Bwana.