Biblica® Open Kiswahili Contemporary Version (Neno) 2015

Zaburi 148:1-14

Zaburi 148

Mwito Kwa Ulimwengu Kumsifu Mungu

1Msifuni Bwana.

Msifuni Bwana kutoka mbinguni,

msifuni juu vileleni.

2Msifuni, enyi malaika wake wote,

msifuni yeye, enyi jeshi lake lote la mbinguni.

3Msifuni yeye, enyi jua na mwezi,

msifuni yeye, enyi nyota zote zingʼaazo.

4Msifuni yeye, enyi mbingu zilizo juu sana,

na ninyi maji juu ya anga.

5Vilisifu jina la Bwana

kwa maana aliamuru navyo vikaumbwa.

6Aliviweka mahali pake milele na milele,

alitoa amri ambayo haibadiliki milele.

7Mtukuzeni Bwana kutoka duniani,

ninyi viumbe vikubwa vya baharini na vilindi vyote vya bahari,

8umeme wa radi na mvua ya mawe, theluji na mawingu,

pepo za dhoruba zinazofanya amri zake,

9ninyi milima na vilima vyote,

miti ya matunda na mierezi yote,

10wanyama wa mwituni na mifugo yote,

viumbe vidogo na ndege warukao,

11wafalme wa dunia na mataifa yote,

ninyi wakuu na watawala wote wa dunia,

12wanaume vijana na wanawali,

wazee na watoto.

13Wote na walisifu jina la Bwana,

kwa maana jina lake pekee limetukuka,

utukufu wake uko juu ya nchi na mbingu.

14Amewainulia watu wake pembe,148:14 Pembe hapa inawakilisha mwenye nguvu, yaani mfalme.

sifa ya watakatifu wake wote,

ya Israeli, watu walio karibu na moyo wake.

Msifuni Bwana.